USIHOFIE BEI, HOFIA UBORA

Habari rafiki

Linapokuja suala la sisi kufikira kuhusu ujenzi jambo la kwanza linalotujia kwenye akili zetu huwa ni bei na mara nyingi bei ndio huathiri maamuzi yetu. Leo mimi mshauri wako naomba nikushauri kitu, acha kuhofia bei, anza kwanza kuhofia ubora.

Thamani ya nyumba yako iko kwenye ubora; umekuwa ni utamaduni wetu kwa sasa moja kwa moja kuulizia huduma fulani itagharimu kiasi gani na kuchagua ya bei rahisi bila kujihangaisha kujua ubora wa huduma na tunasahau kabisa kwamba thamani halisi iko kwenye ubora na sio kwenye unafuu wa bei. Baadaye utakuja kugundua ulihitaji thamani na sio unafuu.

Bei ni hisia za muda mfupi; mara karibu zote mtu akishamaliza kujenga maumivi huisha, swala alijenga kwa gharama gani huwa halina nguvu tena kama matokeo ya alichokijenga. Kama nyumba ina matatizo au mbovu ataumia sana hata kama alijenga kwa bei rahisi lakini kama amepata nyumba bora hujisikia fahari sana bila kujali ilimgharimu kiasi gani. Kabla hujafanya maamuzi jua kwamba bei ni hisia ya muda mfupi na matokeo ndio yatakuja kukuonyesha hilo.

-Rahisi huweza ghali zaidi; unapokutana na kitu rahisi sana ni muhimu kuweka mashaka hasa kwenye kujihakikishia ubora wa hiyo rahisi kwani unaweza kujikuta unakuja kufanya marekebisho yakayokugharimu zaidi ya ile uliyoona ni ghali kwa sababu ulishindwa kuangalia ubora. Tumekutana na kesi nyingi sana za kazi zilizoharibika kwa sababu ya watu kukimbilia urahisi na mwisho wamekuja kuingia gharama kubwa zaidi ya ile waliyoona ni ghali kwa sababu inatulazimu kuwarekebishia baada ya kubomoa, kwa bahati mbaya gharama ya vifaa haibadiliki kwa utofauti wa gharama, gharama ni ile ile.

Tofauti ndogo ya bei isikuletee maumivu ya muda; mara nyingi tofauti kati ya nafuu na ubora sio kubwa ni tofauti ndogo sana na gharama ya vifaa itakayoleta matokeo mabovu ni sawa na gharama ya vifaa itakayoleta matokeo bora. Kumbuka kwamba kujenga ni kama kuoa mke, unajenga jengo litakaloishi angalau miaka 100 mbele na utalokuwa unalitazama maisha yako yote hivyo kama litakuwa halikufurahishi litakukosesha raha kwa kipindi chote cha maisha yako pengine hata kukupunguzia siku za kuishi, kwa hivyo hisia za bei ambazo ni za muda mfupi sana zisikusababishe ukashindwa kufanya maamuzi sahihi na muhimu sana ya maisha yako.

N:B Ubora Ni Jambo Muhimu Sana Linapokuja Suala La Ujenzi Kwa Maana Ujenzi Mbovu Haujifichi Na Ukiharibu Lazima Utajutia Maamuzi Yako. Ninaposema Zingatia Ubora Simaanishi Lazima Ukimbilia Huduma za Bei Kubwa Bila Sababu Bali Namaanisha Kipaumbele Chako Kiwe Ni Ubora Na Sio Gharama, Yaani Usiingie Kwenye Mtego Hisia Za Kusukumwa Na Unafuu Wa Bei Ukasahau Ubora Kwani Mwisho Wa Siku Thamani Iko Kwenye Ubora Na Sio Unafuu Wa Bei Na Mara Nyingi Hilo Utaliona Baada Ya Kuwa Umemaliza Ujenzi. Ni Changamoto Tunayokutana Nayo Mara Kwa Mara Na Mara Zote Inaambatana Na Hasara Kubwa Kwa Upande wa Mhusika/Mteja.

Architect Sebastian Moshi

1 reply
  1. Sisa
    Sisa says:

    Andiko zuri. Ni kweli watu huwaza zaidi gharama kuliko dhamani anayoenda kuipata. Inabidi tubadilike na kutafakari zaidi thamani na ubora kuliku kuweka gharama kama nguzo kuu

    Reply

Leave a Reply

Want to join the discussion?
Feel free to contribute!

Leave a Reply to Sisa Cancel reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *