UJENZI UNAPOKOSA WATAALAMU NA THAMANI INAKOSEKANA PIA.

Siku za hivi karibuni nilifanya kikao na ofisa mmoja wa mikopo wa moja kati ya benki za kigeni zinafanya vizuri sana hapa nchini. Tuliweza kuongea mengi na mimi nikijaribu kumpa maelezo ya mapendekezo yangu kwake ndio tukajikuta tumeingia kwenye mjadala mmoja uoavutia sana. Aliniambia kwamba wamekuwa wakitoa mikopo ya ujenzi kwa mashirika na kwa watu binafsi ambapo pia mikopo hii wamekuwa wakiwapa watu fedha taslim moja kwa moja waende wakajenge wenyewe kadiri watakavyoamua lakini miradi hiyo itakaguliwa kwanza na mthaminishaji wao kabla ya wao kupewa fedha za hatua inayofuata.

Sharti la kupewa fedha ya hatua inayofuata iliamualiwa na ripoti ya mthaminishaji aliyekuwa na kazi ya kuangalia kama ujenzi huo umefanyika kwa viwango vinavyotakiwa. Akaniambia sasa mara nyingi wathaminishaji wamekuwa wakirudisha ripoti ambazo zilipelekea miradi hiyo kusimamishwa na kutoendelea kupewa hela yoyote. Kutokea hapo ndipo benki ikaamua kwamba sasa itakuwa inatoa orodha ya wakandarasi ambapo mteja atachagua mmojawapo kisha benki itamlipa fedha mkandarasi huyo akajenge kwa viwango anavyopangiwa badala ya kumlipa mteja akajiamulie mtu atakayechagua kumjengea.

Mimi nilimuuliza afisa huyo swali moja tu, je miradi hiyo ilikuwa na wataalamu kwenye usimamizi? Alinijibu kwamba wateja wenyewe ndio walijichagulia na mara nyingi hawakutumia wataalam hao. Ndipo nikamwambia kwamba kila kitengo katika tasnia ya ujenzi ina wataalamu waliobobea ambao ni vigumu sana kufanya maamuzi ya kazi inayokwenda kufanyika chini ya viwango. Kufanya ujenzi chini ya kiwango mara nyingi inasababishwa sana na kukosekana kwa maarifa sahihi ya kitaalamu na kufanyika kwa maamuzi mabovu yanayopelekea uharibifu. Hivyo kufanya kazi ya ujenzi bila kuzingatia washauri wa kitaalamu ndio chanzo cha kukosa thamani sahihi inayotegemewa kwenye mradi wa ujenzi kwa sababu ya maamuzi mengi kufanyika chini ya viwango vinavyotakiwa kitaalamu kwa sababu wafanyaji sio wataalamu.

Karibu sana.

Architect Sebastian Moshi.

Whatsapp/Call +255 717 452 790.

0 replies

Leave a Reply

Want to join the discussion?
Feel free to contribute!

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *